Monday, February 29, 2016

SHULE 18 DAR KUNUFAIKA NA ELIMU YA USALAMA BARABARANI

IMG_4204
Meneja wa Volkswagen nchini, Bi. Tharaia Ahmed (kulia) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mafunzo ya elimu ya usalama barabarani ambayo wanataraji kufanya katika shule 18 zilizo katika Manispaa ya Ilala.Mkurugenzi Mtendaji wa CFAO Motors Group, Eric Potin, (katikati) na Mwanzilishi wa mashindano ya mbio za magari ya Go4school, Henning Nathow.
Katika kusaidia kupambana na ajali za barabarani kwa watoto wa shule za msingi jijini Dar es Salaam, kampuni ya CFAO Motors Group kwa kushirikiana na Alliance Autos ambao ni
wauzaji wa magari ya Volkswagen wametoa msaada wa elimu na vifaa vya usalama barabarani kwa shule 18 zilizo katika Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam.
Akizungumzia msaada huo Meneja wa Volkswagen nchini, Tharaia Ahmed amesema kuwa lengo la kutoa elimu na vifaa hivyo ni kuwasaidia wanafunzi wa shule ambao wengi wao wamekuwa hawana uelewa mzuri kuhusu kuvuka barabara.
Alivitaja vifaa hivyo kuwa ni alama za barabarani ambazo zinaonyesha alama za kusimamisha magari ili wanafunzi wavuke, makoti yanayowatambulisha waongozaji, kofia za kuwazuia na jua na mipira ya michezo mashuleni na watatoa elimu katika shule hizo ili kuwasaidia watoto kujua sheria za barabarani.
“Tumeamua kutoa msaada huu kwa shule 18 na tutatoa elimu na tutakabidhi vifaa … tunaamini msaada huu utaweza kuwasaidia watoto hao na tunaamini itasaidia kupunguza ajali barabarani,” alisema Bi. Tharaia.
Akipokea vifaa hiyvo kwa niaba ya Afisa Elimu wa Ilala, Helen Peter alisema wanaishukuru CFAO Motors Group kwa kutambua umuhimu wa elimu na kutoa vifaa vitakavyoweza kusaidia kuongoza wanafunzi wavukapo barabara.
"Tunashukuru sana kwa msaada huu na mmeonyesha ni jinsi gani mnatambua umuhimu wa elimu na sisi tupo pamoja nanyi na tupo tayari kupokea elimu hiyo," alisema Bi. Helen.
Alizitaja baadhi ya shule ambazo zitapata vifaa hivyo kuwa ni Shule ya Msingi Msimbazi, Boma, Mnazi Mmoja, Uhuru Mchanganyiko, Tabata, Ilala, Lumumba, Muhimbili, Buguruni, Kasulu, Mkoani, Msimbazi Mseto, Hekima, Amana, Mtendeni, Buguruni Viziwi na Tabata Jeta na Mtandani.
Pamoja na hayo pia kunataraji kufanyika mashindano ya mbio za magari yaliyo na lengo la kuchangia elimu nchini Rwanda yanayoratibiwa na kampuni ya CFAO Motors Group yanayofanyika nchini na yanataraji kumalizikia nchini Rwanda.
Attu Mynah
Meneja Masoko wa CFAO Motors Group nchini, Bi. Attu Mynah (kulia) akionyesha baadhi vifaa hivyo vya usalama barabarani kwa waandishi wa habari (hawapo pichani).
Mbio hizo za kusaidia elimu nchini Rwanda zimepewa jina la The go4school Charity Rally ambazo zimeshirikisha magari 18 ambayo yameanzia jijini Dar es Salaam na yanataraji kufikia kilele chake Machi, 13 nchini Rwanda na yatapita katika nchi za Kenya na Uganda na kisha Rwanda.
Akizungumzia mashindano hayo Mkurugenzi Mtendaji wa CFAO Motors Group, Eric Potin alisema mbio hizo za magari zimeanzishwa na taasisi ya Volkswagen kwa kushirikiana na taasisi ya Opportunity International Germany kwa kutambua kwao umuhimu wa elimu na usalama wa watoto wawapo barabarani.
Alisema kuwa wamekuwa wakisaidia zaidi katika sekta ya elimu na sio mara ya kwanza kufanya mbio hizo za magari kwani mwaka 2013 walifanya mbio kama hizo kutokea Senegal hadi Ghana na mwaka 2015 walifanya kutokea Namibia hadi Malawi na mara zote kampuni ya CFAO Motors Group imekuwa ikihusika kufanikisha mbio hizo.
Henning Nathow
Mwanzilishi wa mashindano ya mbio za magari ya go4school, Henning Nathow (wa pili kushoto) akielezea dhumuni lengo lao la kusaidia upatikanaji wa elimu bora kupitia mradi wa go4school.
“Mbio hizi zimeanzishwa na Wajerumani ili kusaidia elimu ya Rwanda na hii sio mara ya kwanza tayari yamefanyika mara mbili barani Afrika na sisi kama CFAO tumekubali kuungana na taasisi ya Opportunity International Germany ili kusaidia upatikanaji wa elimu,” alisema Potin.
Nae Henning Nathow ambaye ndiyo mwanzilishi wa mradi wa go4school ulio na lengo la kusaidia upatikanaji wa elimu bora alisema wanafurahi kufanya mbiao hizo ambazo zina lengo la kusaidia elimu nchini Rwanda wa wanaamini elimu ndiyo njia pekee inayoweza kusaidia kupambana na umasikini.
Alisema wanataraji kufanya mbio hizo na baada ya kufika Rwanda watayakabidhi magari yanayotumika kwa ofisi za CFAO za Rwanda na baada ya hapo watayauza na mapato yatakayopatikana watayakabidhi kwa serikali ya Rwanda ili kusaidia sekta ya elimu.
“Elimu ni njia ambayo inaweza kusaidia kumaliza janga la umasikini na sisi tuna furaha kufanya mbio hizo kuelekea Rwanda ili kusaidia kupatikana kwa elimu bora Rwanda,” alisema Nathow.
Helen Peter
Afisa Elimu wa Ilala, Helen Peter akitoa neno la shukrani kwa kampuni ya CFAO Motors Group kwa msaada huo wa vifaa vya usalama barabarani kwa shule 18 zilipo ndani ya Manispaa ya Ilala.
Eric Potin
Mkurugenzi Mtendaji wa CFAO Motors Group, Eric Potin (wa pili kushoto) akimkabidhi Afisa Elimu ya Ufundi wa Manispaa ya Ilala, Bi. Helen Peter (wa kwanza kushoto) msaada wa vifaa vya usalama barabarani kusaidia wanafunzi wavukapo barabarani pamoja na vifaa vya michezo, Wanaoshuhudia tukio hilo ni Meneja wa Volkswagen nchini, Bi. Tharaia Ahmed na (kulia) na Meneja Masoko wa CFAO Motors Group nchini, Bi. Attu Mynah.
Eric Potin
Attu Mynah
Meneja Masoko wa CFAO Motors Group nchini, Bi. Attu Mynah akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani).
Volkswagen Tanzania
Pichani juu na chini ni kati ya magari 18 yaliyoondoka nchini jana kuelekea Rwanda kwa ajili ya kushiriki mashindano ya mbio za magari yaliyo na lengo la kuchangia elimu nchini Rwanda yanayoratibiwa na kampuni ya CFAO Motors Group.
Volkswagen, Tanzania
IMG_4332
Msafara wa magari aina ya Volkswagen yanayoelekea nchini Rwanda yakitoka kwenye 'showroom' ya Volkswagen iliyopo kampuni ya CFAO Motors Group, barabara ya Pugu jijini Dar.
Volkswagen Tanzania

No comments: