Saturday, August 11, 2007

CHAHALI, VYA KUMUNG’UNYA UNATAFUNA, INAKUWAJE?

Na Tulizo Kilaga
(MAKALA MAALUM KWENYE GAZETI LA RISASI -AGOSTI 11,2007)

JUMATANO ya wiki hii, yaani Agosti 8, 2007 nilisoma, nikashtuka, nikapata uchungu kutokana na makala iliyoandikwa na Evarist Chahali, iliyokuwa na kichwa cha habari ‘Magazeti ya Udaku yanaandika habari feki’. Nililazimika kusoma makala hayo zaidi ya mara tano na kila nilipofika kwenye neno “ shame on you!” niligadhabika na kutafuta nguvu ya kujenga hoja, hatimaye nikajiridhisha na sasa naomba niweka sawa haya yafuatayo.

Evarist Chahali amedhihirisha wazi kuwa ana uelewa mdogo katika uandishi, anadhani kujua kusoma na kuandika pekee kunatosha mtu kuwa mwandishi, najua wapo wengi wasioamini kuwa uandishi ni taaluma kama huyu mkurupukaji Chahali, hivyo nataka niwathibitishie kuwa uandishi ni taaluma.

Binafsi nimefadhaishwa sana na maneno nitakayoyanukuu hapa chini kutoka kwenye makala yake “Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndiyo kuwafanya watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli? Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli, sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari? Shame on you!”

Mwandishi huyo amesahau kuwa Risasi ni gazeti lenye jukumu kubwa la kuhakikisha linaipa jamii habari iliyo sahihi na ya kuaminika.

Nikiwa kama mhariri msaidizi wa gazeti hili, nasema Chahali ni muongo! Amenisikitisha kwani mtu mzima kuanza kuzusha na kusema uongo kwa faida ya vitu vidogo vidogo vyenye shibe ya kitambo, ni mambo ya kuhuzunisha na kujidhalilisha.

Mimi nasema kuwa, Chahali kwa elimu yake kubwa, alipaswa kujua kuwa katika kutoa hoja mtu anatakiwa kufuata taratibu za fikra sahihi na si vionjo kama alivyofanya!

Nakumbuka vema katika miaka mitatu niliyokesha kutafuta Shahada yangu ya kwanza katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Tumaini- Iringa Mkufunzi wangu wa Physchologia Marehemu Prof. Samuel Mshana (Mungu amlaze mahala pema peponi) alipenda kunisisitizia maneno ya mwanafalsafa Plato kuwa ulimwengu umegawanyika katika makundi mawili, yaani ulimwengu wa busara na akili na ulimwengu wa muonekano/maoni.

Kimsingi Plato anamaanisha kuwa wale wenye busara na fikra sahihi wapo kwenye ulimwengu wa ukweli na wale wenye vionjo kama Chahali wapo kwenye ulimwengu wa maoni!

Chahali ni mchangiaji wa habari katika gazeti la Kulikoni anayeishi Scotland, nchini Uingereza ambako anasomea Udaktari wa Falsafa katika Siasa za Kimataifa, hususan kuhusu Afrika na anafanya utafiti kuhusu Uislam na harakati za vikundi vya Kiislam nchini Tanzania.

Huyu ni msomi kwani alipata Shahada ya Kwanza katika Elimu ya Jamii Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ‘Mlimani’ kabla ya Kupata Shahada ya Uzamili katika Siasa na Uhusiano wa Kimataifa kisha kufuatiwa na Shahada ya Uzamili wa Utafiti (Master of Research-MRes) katika Utafiti wa Siasa (Political Research) huko aliko sasa.

Hakika Chahali ni msomi lakini kuna maswali mengi najiuliza, hivi huyu ni msomi wa aina gani, anayethubutu kuandika makala bila kuifanyia uchunguzi? Mbaya zaidi ndugu yangu ana taaluma ya Shahada ya Uzamili wa Utafiti, lakini hataki kwa makusudi kuitumia! Msomi wa namna hii ni sawa na mwandishi asiyeweza kuona mwanga gizani.

Nakumbuka siku namaliza shahada yangu ya uandishi wa habari, mkufunzi wangu aliyekuwa akinifundisha ‘teaching methodology’ Fredy Nyamubi aliniambia kuwa, ili ujue elimu uliyonayo inakusaidia ama umeelimika lazima uweze kutumia taaluma ulionayo katika maisha yanayokuzunguka. Hivyo, kila ninapotaka kufanya kazi zangu huyakumbuka maneno haya.

Chahali anapaswa kujua kuwa, zipo kanuni zinazomuongoza mwandishi yeyote kuweza kupata habari iliyo sahihi, hivyo ukitumia vema kanuni hizo pamoja na mambo kadhaa ya msingi yanayoifanya habari kuwa habari, basi habari itakayoandikwa huwa sahihi.

Tasnia ya habari duniani kote huzingatia kanuni nne ambazo ni ukweli, utii, uthibitisho na kuwa na imani na unachokiandika, hivyo Chahali lazima azingatie kanuni hizi, lakini kwa kuwa watanzania hawana utamaduni wa kujisomea wanaweza kupata Gazeti la Rai la Alhamisi ya Juni 28 – Julai 4, 2007 Uk. 9 ambapo kuna makala iliyoandikwa na mkongwe wa habari, Muhingo Rweyemamu.

Katika makala hiyo Rweyemamu anasema “Uandishi wa habari una tofauti na uandishi wa barua au malalamiko. Anayelalamika hata kama analalamika kwa rais, hana sababu ya kumpa nafasi anayemlalamikia vivyo hivyo kwa mwandishi wa barua.”

Nirudi kwa Chahali, hivi ni kweli hajui kuwa nidhamu ya msingi ya mwandishi wa habari duniani kote ni ile inayompa nafasi mtuhumiwa? Sitaki kuamini kuwa nawe ni miongoni mwa watu wanaoamini nidhamu hii huitajika kwenye habari kubwa ya kuuzia gazeti tu! Hata makala hutakiwa kuzingatia hili kwani nayo ni habari.

Hainiingii akilini, kwanini Chahali hakutaka kutoa nafasi kwa wahariri wa gazeti hili ili kujua ukweli wa habari iliyochapishwa katika toleo na. 400 la Julai 18-20 yenye kichwa cha habari “ Warembo TZ wapiga picha za x tupu? Anadai kinachomsikitisha siyo kama habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika.

Chahali anaamini kuwa anajua kila kitu! Jambo ambalo siyo kweli na haliwezekani.

Hata hivyo, nataka nimfahamishe kuwa habari inayoandikwa na mwandishi anayejifanya kuwa na taaluma zote kichwani ina madhara makubwa kwa jamii kwa sababu huweza kumuumiza mtu ama kumsababishia kifo.

Hivi Chahali alitaka tuambatanishe na mtandao wanaopatikana warembo hao ili athibitishe kuwa ni watanzania? Haoni kuwa kwa kufanya hivyo ni ‘kuwapromoti’ mabinti hao? Kama kulikuwa na ulazima kwanini yeye hakuweka bayana mtandao aliodai kuwa alitumiwa na rafiki yake uliokuwa ukikanusha habari yetu?

Nawaheshimu sana watanzania na siwezi kamwe kuwafanya wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli! Nataka kuwathibitishia watanzania wote kuwa RISASI ni gazeti linalozingatia kanuni na maadili ya uandishi wa habari.

Baada ya kusema hayo, naomba niweke wazi ‘link’ za mtandao ambao kila mwenye nafasi aweze kuupitia ili kuona nani ni muongo kati ya Chahali na Gazeti la Risasi. Mtandao huo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambapo wote wanadai ni wakazi wa Dar es Salaam, Tanzania sasa Risasi limedanganya nini?

Kimsingi simkatazi Chahali siku nyingine kuandika maoni yake, kwani maoni ni miongoni mwa njia za kupata ukweli, lakini mara unapoupata unapaswa kuhakikisha unaufuata!

Kama Chahali alikuwa hajui basi nichukue nafasi hii kumfahamisha kwa ufupi kuwa, kuna baadhi ya mambo ambayo hufanya habari kuwa habari ‘elements that make news to be newsworthiness’ ambazo ni kama zifuatazo.

Kwanza kabisa kuna (proximity) ukaribu wa habari husika na jamii lengwa, (prominence) inamhusu mtu gani maarufu, (impact) madhara ama umuhimu wake kwa jamii, (conflict) mkingamo wa mawazo, (timeliness) limetokea lini, (novelity) je tukio hilo ni la kawaida ama si la kawaida na (human interest) uvutaji wa hisia za watu.

Kutokana na sifa hizo ni ukweli ulio wazi kuwa wahariri wa gazeti la RISASI tulikuwa na kila sababu ya kutoa habari ile kwani tukio lenyewe si la kawaida katika jamii yetu labda Chahali anaona ni jambo lisilowezekana kutokea nchini kwetu na kusahau kuwa tukio hilo ni moja ya athari za utandawazi.

Sitaki kutumia muda mwingi kuelezea sifa zote zilizosababisha kuchapisha habari hiyo ila kimsingi Chahali ni miongoni mwa watu wanaosemwa na mwanafalsafa wa siku nyingi, Permanides kuwa kuna watu wanachanganya kati ya ukweli kadiri unavyojitokeza kwao na ukweli halisi na kusisitiza kuwa ni vizuri kuangalia kitu kama kilivyo na si vinginevyo.

Tanzania ni nchi yetu na tuna jukumu kubwa sana mbele yetu katika dunia hii tuliyopo ya ‘information age’ ambalo ni kuhakikisha tunaandika habari za uhakika ili kuiwezesha jamii yetu kupata maisha bora! Sasa kaka Chahali, vya mung’unya, unatafuna, inakuwaje?

Kuna kila sababu ya uongozi wa gazeti hili kuamini kuwa Chahali aliamua kutuchafua ili aweze kupata umaarufu kwani alijua kuwa akifanya hivyo ataandikwa sana na magazeti hivyo, kuanzia hapo atajulikana kwani tangu mwaka 2006 hadi sasa ana watu 2000 tu waliotembelea blog yake, wakati watanzania wengine hupata watu zaidi ya 500 kwa siku.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa namba +255 0715 888887. mwakilaga.blogspot.com

7 comments:

Anonymous said...

taarifa zako zimetoka hapa. Hebu angalia na hizi hapa.

Anonymous said...

..hawa wasitake kutuyumbisha kabisa kwa vile wana vyombo vya habari vya kuongea ili umma uwasikie!hawa jamaa mpaka sasa hawataki kukubali ukweli kuwa wamechamka!yaani hata maoni ya watu hawaangalii kuwa yameelekwezwa wapi bado wanabakia kuja na mihabari yao katika kujitetea!tushwachoka sasa!ila ukweli utabaki pale pale kuwa mmeleta habari feki!watanzania sio wajinga kabisa kukaa na kuwasikiliza nyie tu kwani mmekuwa nani?watu hapa wanakuja na vyanzo vingine vya habari mbona mmekaa kimya tu!hawa wadada nina uhakika kabisa ni wamerekani na sio watanzania kama mnavyodai na kuendelea kujitetea kuwa ni watanzania!nawashangaa sasa nyie kwa kukubali haraka tu kuwa ni watanzania kwa kuona location yake ni Dar es salaam. Je kwani ni watu wangapi wanaweka miji mingine na wakati wao ni watanzania??sijui mna habari na hilo???na pia mnafahamu kuwa hi 5 kuna suala la Location na Hometown???na ukiachilia yote hayo pia suala linabakia kuwa mtu anaweza kudanganya katika yote hayo!sasa kwa vile ni mweusi basi ndo mtanzania!acheni kutuletea habari ambazo hata nyie hamuwezi kusema kuwa mna ukakika ya mia kwa mia!kisa tu location yake!tupeni hoja za msingi sio kujisifia na elimu zenu za uandishi wa habari na kuona wengine hamnazo!kwani nyie nani?

Anonymous said...

Hahaha hahaa mtenda akitendewa hujihisi kaonewa.

Mla kunde husahau ila mtupa maganda hasahau.

Ukweli unaumaaaaaaa!!! kama mnavyoumiza wenzenu roho na leo zamu yenu, malipo ni duniani akhera kwenda kuhesabu, mtalipwa hapa hapa na bado akhera mnasubiriwa.

kwani katika imani ya kiislam inasema ukiona jambo lina kheri mbeleni fanya na kama halina kheri basi acha, nyie tangu muanze kuandika habari za watu mshaua watu wangapi kwa pressure, mmeshachanisha ndoa ngapi? mshawafitini watu wangapi? je nyie mko sawa? au mnapata faida gani hata mkituhabarisha kuwa kuna watz wanapiga za uchi?

Hongera Chahali keep it up!!!!!!!!!!!! Mwenyezi mungu atakulinda.

Anonymous said...

big up chahali, hawa jamaa wa GP wanapenda sana umbea, tumechoka kudanganywa kwa mambo ya kuzua, tumeshang'amua kuwa habari zenu nyingi ni za uzushi na umbea, iko siku na nyie yatawarudia!!!!!!!!!!!!!

Anonymous said...

Mwakilaga,
Umetumia muda mwiiingi na makala ndeefu kutetea picha mbazo sooner or later mtabidi kukubali kuwa mmezitoa kwenye mtandao?

Anonymous said...

nimefuatilia kwa kina sana habari zako bro .mrisho,(kuhusu habari hii feki) na nimegundua yafuatayo..unakuja kwa gia ya kuandika habari ndefuuu ili umzuge msomaji na akuone wewe ni mkweli,pili,unatumia muda mwingi kumsema mtu 'personally' mara wa mwisho darasani,mara elimu yake feki,mara ooh blog yako inaembelewa na watu wachache(watu 2000 tu tangu mwaka 2006) nk badala ya kuleta hoja za kimsingi kuhusu utoaji wa habari hiyo,tatu,anatumia mzunguko mrefu kuelezea kanuni za kiuandishi yani kama tupo 'class' vile,wakati wasomaji hatuziitaji sana bali tunataka kujua ukweli ni upi kuhusu habari ile,nne,unakomaa na unaforce chanzo chako kilicho feki(hi5)wakati ukweli unaujua kwamba ile ni friends web inayotumika na kila mtu with no limits katika 'kuupload na kuupgrade na kuedit' vitu..na katika uandishi wako umecomplain kwamba chahali hajaweka website hiyo aliyodai kuwa ni chanzo cha zile picha(sasa kwa taarifa yako hiyo web tayari bwana chahali kaiweka ni kazi kwako sasa!)isitoshe mr kichuguu nae kakupa link yako na ile "original" kazi kwako kunyoa au kusuka ..kukubali au kukana,kuomba radhi kwa umma na chahali au kuuchuna....na ujue kukubali kwako kuwa ile ni feki nadhani moto utawaka na tunalisubiri hilo...by erwin fom india

Anonymous said...

sijaona sababu ya TULIZO KILAGA kusema yeye ni muhitimu wa TUMAINI UNIVERSITY!!!!