Monday, December 28, 2009

WIKIENDA SHOWBIZ!

NANI ALIFUNIKA, NANI: ALICHEMKA 2009?
2009 ulikuwa ni mwaka kinyumenyume na kimbelembele kwa wakati mmoja. Mastaa wengi wamefunikwa, wapo walioongeza mvuto wao kijamii, wapya kibao lakini pia hawasahauliki wale waliolinda majina yao kutokuporomoka.

INGIZO JIPYA
Belle 9 amesimama sawasawa, big up little brother. Dogo ameweza kufanya R&B ya ukweli na kukonga nyoyo za wadau, kipaji chake hakipingiki, sauti yake haina ganzi, yupo juu.

Steve amesimama mwaka huu, ingawa hapa tunapoelekea kumaliza mwaka ni kama amenyamaza. Hapo katikati alifanya vizuri na kibao chake Sogea Karibu ambacho amemshirikisha Dataz na kuitawala R&B kwa kipindi kirefu.
Bwa’ mdogo Barnabas ambaye ni zao la THT, ameng’ara na kutoka vizuri, alianza na Pipi kwa kibao chao Njia Panda, baadaye akaendelea na miradi mingine na kuzidi kusimama.

Dogo mwingine anayeitwa Diamond, naye amefanya vizuri hasa katika kipindi hiki ambacho mwaka unaelekea kuisha.

Pascal Cassian ndiye mshindi wa Bongo Star Search mwaka huu, ingawa tangu alipokabidhiwa taji, hajasikika katika mradi mwingine, inawezekana anajipanga.

Mbali na Pascal, wakali wengine kama Peter Msechu, Kelvin Mbati na Beatrice William, wameweza kuibuliwa na BSS, hivyo ni wao na spidi zao ili kukwea matawi ya juu.

Illuminata ni mshiriki wa Project Fame mwaka huu kutoka Tanzania ambaye alijitahidi kufikia nafasi nzuri, katika shindano hilo msimu wa tatu ambapo Mnyarwanda, Alpha alishinda.

WALIOENDELEA KUNG’ARA
Laurence Malima ‘Marlaw’, mwaka huu ameendelea kuthibitisha kuwa kwenye fani, tangu alipotoka mwaka 2006 yeye ni zaidi ya madini, kwani bado ameng’ang’ania kwenye chati mpaka mwaka mwingine unakatika.

Ali Saleh Kiba ‘Alikiba’, bado ni lulu ya biashara kwenye muziki wa Bongo Flava, kibao chake cha Usiniseme, kinaheshimiwa kitaani kama vile wimbo wa taifa. Haya ni mafanikio makubwa, kwani tangu mwishoni mwa mwaka 2006 alipotoka, bado yupo juu.

Hamis Mwinjuma ‘FA’, yupo sawa, mwaka unakatika yupo juu, ingawa ilidhaniwa kuwa angefunikwa kwa sababu ya kuwepo masomoni nchini Uingereza.
Ambwene Yesaya ‘AY’ bado kamili kwenye fani, amethibitisha kuwa yeye ndiye mfalme wa commercial Bongo, huku traki yake Leo ambayo ameifanya katika version mbalimbali ikimvusha level nyingine.

Joseph Osmund Mbilinyi ‘Mr. II’ alikuwa kimya, lakini Desemba imesababisha awe gumzo, traki yake Hold On imekubalika kitaani, na ni wiki iliyopita alizindua albamu yake ya 10 inayokwenda kwa jina la Veto.

Jaffari Ali Mshamu ‘Jaffarai’ ni kichwa kingine ambacho kimesimama vizuri, ameweza kufanya mradi wake binafsi, pia amesababisha Wateule kusikika upya.
Msafiri Kondo ‘Solo Thang’, ameweza kuwakumbusha Watanzania kwamba yeye bado ni mtaalamu wa mashairi ya Hip Hop, katika verse ya mwisho ya wimbo Msela ambayo ameifanya yeye, amefunika vibaya, pia sauti yake ipo kwenye albamu ya Sugu, Veto ndani ya wimbo Bunduki.

Joseph Haule ‘Prof Jay’, bado amesimama, nyimbo zake alizozifanya mwaka jana, bado zimeendelea kusikika, lakini kubwa ni sauti yake kwenye wimbo Nazeeka Sasa wa FA ambao umemfanya aendelee kutuwama kwenye chati.

Abdul Sykes ‘Dully’ naye ameendelea kukaa kwenye chati, licha ya game kukumbwa na mtikisiko wa kimapinduzi kutoka kwa damu changa. Wimbo wake wa Shekide ambao aliufyatua muhula wa pili wa mwaka huu, mempa chati.

John Simon ‘Johmakini’ ameendelea kuthibitisha yeye ni kichwa cha kuandika na swagger za Hip Hop anazijua, amefanyakazi nyingi nzuri na kuendelea kung’ara.
Makundi ya Wanaume Family na Tip Top Connection yamefanya vizuri hasa baada ya kuungana na kufanyakazi pamoja. Wasanii wake, Madee, Tundaman, Mh. Temba na Chege wameweza kung’ara katika miradi binafsi.

Staa wa Hip Hop, Rashid Makwilo ‘Chid Benz’ bado ameendelea kutetea kiwango chake na kwa mwaka huu, bado amesimama.

Kundi la Offside Trick na kibao chake Pole Samaki limetoka vizuri, wakati msanii wa kundi hilo, AT akimrudisha vizuri mkongwe Stara Thomas kupitia wimbo wake Nipigie.

Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ na Machozi Band, ameendelea kuwa staa wa Afro Pop.

Hemed Suleiman baada ya kutoka Project Fame mwaka jana, alikaa kimya lakini mwaka huu aliamka na kuthibitisha kuwa ushiriki wake haukuwa wa wasiwasi, alitoa kibao kinachoitwa Ninachotaka na kupakua cha pili kilichofunika, Ulisema.

WALIORUSHA MIGUU
Mkongwe Haroun Kahena alijitahidi kurusha miguu, wimbo wake Haina Ngwasu ni mkali, lakini haukupata air play ya kutosha, kwahiyo ukosefu wa promo unamfanya tumuweke katika kundi la waliorusha miguu.

Rehema Chalamila ‘Ray C’ naye alijitahidi kurusha miguu lakini bado hajaweza kusimama. David Nyika ‘Daz Baba’ na kundi lake la Watanzaniano nao ni hivyo hivyo, kama ilivyo kwa Ferouz Mrisho na Juma Kassim ‘Sir Nature’ ambao pamoja na kuzindua albamu, lakini bado hawajarudi kwenye chati zao.

WALIOSHINDWA KABISA
Wapo ambao imeshindikana kurudi, Sister P, Zay B, JI a.k.a Kidato Kimoja, Gwamaka Kaihula ‘GK’, Karama Bakari ‘Luteni Kalama’, Karama Masoud ‘Kalapina’, Mandojo & Domokaya, Suleiman Msindi ‘Afande Sele’ na wengineo wengi wameshindwa kurejea katika chati zao za zamani.

FILAMU
Yusuf Mlela amefunga mwaka vizuri, hasa baada ya kuibuka Ijumaa sexiest Bachelor 2009, amefanyakazi nyingi na kung’ara katika fani hiyo.
Hemed mbali na muziki, pia anaonekana kwenye filamu, kwani mwaka huu umekuwa mzuri kwake, kama ilivyo kwa Yusuf. Hemed ni mmoja wa wanafainali wa Ijumaa Sexiest Bachelor.

The Big Two, Vincent Kigosi ‘Ray’ na Steven Kanumba wameendelea kuthibitisha kwamba wao kwenye filamu ni ngumu kuzima moto wao.
Single Mtambalike ‘richie’, Jacob Steven ‘JB’, Irene Uwoya, Wema Sepetu, Aunt Ezekiel na wengineo wengi wameweza kufanya vizuri.

WATAYARISHAJI WA MUZIKI
Marco Challi wa MJ Records amefanyakazi nyingi, akifuatiwa na Lamar lakini Hammy B, yeye anaingia katika orodha kwa sababu katika kazi chache alizofanya, zote ni kali na zilisimama.

**************************************

Sugu:Adondosha Veto ‘street
Baada ya kuzindua albamu yake ya 10 kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam wiki iliyopita, mkongwe Joseph Mbilinyi ‘Mr. II’ tayari ameiingiza sokoni santuri hiyo yenye jina la Veto ambayo ina jumla ya mawe 10 ya adabu.

Mr. II a.k.a Sugu, aliingiza albamu hiyo juzi (Jumamosi) na amesema kwamba kazi hiyo itauzwa kwenye maduka ya wazalendo nchi nzima.

“Mapambano yanaendelea, albamu ipo mtaani sasa,” alisema Sugu, alipoongea na kona hii, wikiendi iliyopita, kwa njia ya simu.

Albamu hiyo, imetengezwa nchini Marekani chini maprodyuza Puzo na Stigo katika Studio ya S&S iliyopo mjini Brocklyn.

Baadhi ya wasanii walioingiza vocal kwenye kazi hiyo ya Sugu ni Prof. Jay, MwanaFA, Balozi Dolla Soul, Solo Thang na wengineo.

Mbali na hilo, Sugu alisema nasi kwamba video ya Hold On tayari imekwishaanza kuchezwa na vituo vya runinga na kueleza kuwa imegharimu zaidi ya dola za Marekani 8000.
*****************************************

MYA:Hawa ndiyo vidume aliowaonjesha penzi!
Wakati Abby Cool & MC George over the weekend ikielekea kumaliza mwaka, Ebwana Dah inamuanika staa anayefunga mwaka 2009 kabla ya kuanza na wengine 2010.

Yakiwa ni maombi ya baadhi y wasomaji na wapenzi wa safu hii, mwanamuziki M’ya Harrison ndiye anayefunga pazia la 2009 na kama kawaida, hapa inawekwa orodha ya wanaume ambao kwa nyakati tofauti amehusika nao katika sanaa ya faragha a.k.a mapenzi.

Kwa mujibu wa mtandao ‘unaodili’ na umbea wa staa gani katoka na nani huko kiwanja, mwanaume wa kwanza ambaye anatajwa kuhusika na M’ya ni Cam`ron, ingawa haitajwi ni lini walibanjuka.

Staa wa Hip Hop, The Game anatajwa wa pili katika orodha hiyo, lakini kama ilivyo kwa Cam’ron, haielezwi ni lini walianza kuonjana na ni siku gani waliwekana pembeni.

Hata hivyo, Silk The Shocker ndiye pekee anayeelezewa kwa kipindi, kwamba alianza kujikunja naye mwaka 1996 na mwaka 2000 kila mmoja alishika hamsini zake.

Jina lake kamili ni Mýa Marie Harrison, alizaliwa Oktoba 10, 1979, Washington, District of Columbia, Marekani. Umri wake ni miaka 30. Ni mhitimu wa shule ya Eleanor Roosevelt High Schoo, dini yake ni Mkristo.
****************************************

Joyce Kiria kujiachia na watoto yatima
Presenta wa Bongo Movies kupitia Kituo cha Runinga cha East Africa cha jijini Dar, Joyce Kiria Nkongo ‘Stering’ ana plan ya kukusanya watoto yatima kutoka vituo mbalimbali vya jijini na kujumuika nao katika tamasha linalokwenda kwa jina la watoto wa baba litakalofanyika Januari Mosi.

Akichonga na safu hii, Joyce ambaye ndiye mratibu wa ishu hiyo amedai kuwa shoo hiyo itakayojumuisha mastaa mbalimbali wa Bongo Flava na Movies itafanyika Tabata katika Kituo cha Hot (Help Opharn Tanzania) ambapo watoto kutoka vituo mbalimbali watakutana hapo na kusherekea mwaka mpya kwa pamoja.
****************************
compiled by mc george

No comments: