Friday, December 18, 2015

RAIA WANNE WA CHINA WAHUKUMIWA MIAKA 20 JELA

Watuhumiwa wakifikishwa mahakamani .

Pembe za Faru walizo kamatwa nazo watuhumiwa hao wanne rai wa China katika Mpaka wa Kasumulu Kyela.
Na Ezekiel Kamanga, Mbeya.Jamiimojablog

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi mkoa wa Mbeya imewahukumu kifungo cha miaka 20 jela raia wanne wa China na kulipa faini  baada ya kukutwa na hatia kwa makosa matatu ikiwemo uhujumu uchumi kwa kukutwa na pembe za faru.


Kabla ya kuanza kusoma hukumu Hakimu mfawidhi Michael Mteite alianza kuwashukuru Mawakili wa Serikali na Utetezi pamoja na Mkalimani Manfred Lyoto kwa ushirikiano waliompatia na kuimaliza mapema kesi hiyo kwa siku 23 tu ambapo ameweka historia yeye akiwa Hakimu Mfawidhi kwa kuimaliza kesi kwa muda mfupi.


Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi mfawidhi wa Mahakama hiyo, Michael Mteite aliyeanza majira ya saa tano asubuhi na kuahirishwa mara mbili na kukamilika saa tisa na nusu alasiri ambapo alisema mahakama imeridhika pasipo shaka kutokana na ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka katika makosa yaliyokuwa yakiwakabili watuhumiwa hao.

Mteite alisema Mahakama ilijikita katika kiini cha makosa yote matatu ambayo ni kupanga kutenda kosa kinyume cha sheria la uhujumu uchumi, kufanya shughuli za nyara za serikali kinyume cha sheria ya utunzaji ya wanyama pori inayosomwa pamoja na sheria ya uhujumu uchumi ambapo watuhumiwa waliingiza pembe 11 za Faru bila kibali.

Alisema kosa la tatu ni kupatikana na nyara za serikali kinyume cha sheria chini ya sheria ya uhifadhi ya wanyamapori inayosomwa pamoja na sheria ya uhujumu uchumi ambapo maeklezo ya washtakiwa walikamatwa wakiwa wanamiliki nyara za serikali bila kibali cha Mkurugenzi wa wanyama pori.

Hakimu Mkazi aliendelea kusema ingawa Washtakiwa weote kwa pamoja walikana mashtaka lakini ushahidi upande wa Jamhuri uliuokuwa na mashahidi tisa wate walieleza namna watuhumiwa walivyohusika na kosa hilo.

Alisema uchambuzi wa awali uliofanywa na Mahakama washtakiwa walikubali kwamba wamesimama mahakamani wakikabiliwa kwa makosa matatu, washtakiwa wa pili, tatu na nne walikubali kukamatwa Kyela mjini na kurudishwa mpakani.

Kwa upande wake mwendesha mashtaka wa Seriakali Wankyo Simon akisaidiwa na Archiles Mulisa walisema Washtakiwa hawana kumbukumbu ya makosa ya nyuma ingawa makaso yao yanaonekana yalikuwa yakitendwa kwa kasi kubwa na wanyama pori wamekuwa wakiathiriwa kiasi kwamba vizazi vijavyo vitakosa kuona hazina ya wanyama kwa kuwa watakuwav wametoweka.

Alisema washtakiwa ni raia wa kigeni lakini walikuja nchini kwa lengo la kufanya utalii katika Mlima Kilimanjaro lakini kumbe nyuma ya pazia kuna jambo walikuwa wamelipanga hivy Mahakama inapaswa kutoa adhabu kali ili iwe onyo kwa wengine wenye nia ya kufanya uovu kama huo.

Alisema Mahakama inapotoa adhabu izingatie kifungu cha 86,1,2 C (ii) cha sheria ya Uhifadhi ya wanyama pori  na kwenye kosa la tatu izingatie kifungu cha 5 cha mwaka 2009 na kosa la kwanza kla uhujumu uchumi izingatie sura ya 200 kwani wamevunja mkataba wa kimataifa wa kutunza wanyama walioko hatarini kutoweka.

Alisema Mahakama pia izingatie kifungu cha 85 1(b) na (h) ya sheria ya uhifadhi wanyama pori kwamba nyara zilizokamatwa zinakuwa mali ya serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania sambamba na vifungu vya 111, 1(a), (e) kwamba chombo kilichotumika kinataifishwa na kuwa mali ya Serikali sawa na kifungu cha 111(4).


Pia Wankyo Simon ameiomba Serikali kupitia Mahakama kuwapa tuzo watumishi wa umma waliowezesha kupatikana kwa nyara hizo na kuokoa raslimali za Taifa wakiwemo Maafisa Forodha na Askari wa Jeshi la Polisi.



Aidha Mteite ameiambia Mahakama kuwa Gari namba T 103 DER mali ya Mtuhumiwa wa kwanza Song Lei likabidhiwa Serikalini na simu za watuhumiwa zitauzwa na Mahakama hiyo na nyaraka nyingine zitakabidhiwa kwa upande wa Mashitaka.


Awali Wakili wa Utetezi Ladislaus Rwekaza aliiomba mahakama kuwapunguzia adhabu washtakiwa kwa kuwa ni mara yao ya kwanza kutenda kosa, pia ni raia wa kigeni pia ni vijana wadogo ambao ni nguvu kazi inayotegemewa na taifa lolote.

Hakimu Mteite alisema katika hukumu yake amezingatia maombi ya pande zote zote mbili na kwamba hakuna ubishi kuwa wanyama wanauawa na kuisababishia serikali inaingia gharama kubwa kuhifadhi wanyama pori ili kunusurui wanyama kutoweka.

Alisema katika kosa la kwanza la uhujumu uchumi washtakiwa wanahukumiwa kifungo jela miaka  15 kila mmoja, kosa la pili kwa mujibu wa kifungo cha 83,84(1) washtakiwa wataenda jela kila mmoja miaka 3 na faini ambayo ni gharama ya  mara mbili ya mali waliokutwa nao hivyo watapaswa kulipa Dola za kimarekani 836000.

Alisema katika kosa la tatu kifungu cha 86, 2( c ) inawataka washtakiwa kutumikia kifungo cha kuanzia miaka 20 hadi 30 lakini Mahakama inawahukumu miaka 20 jela na kulipa faini ya fedha ambayo ni mara kumi ya mali waliokutwa nayo ambapo watalipa dola za kimarekani 4180000.

Alihitimisha kwa kusema Washtakiwa kila mmoja atatumia adhabu zote kwa pomoja ambayo ni miaka 20 samba mba na faini zilizoorodheshwa.

Alisema watuhumiwa wanahaki ya kukata rufaa kama wataona wameonewa katika hukumu iliyotolewa na mahakama hiyo.

Washtakiwa waliohukumiwa kifungo cha miaka ishirini ni pamoja na  Song Lei, Xiao Shaodan, Chen Jinlian na Hu Liang ambao walikamatwa Novemba 6, mwaka huu mpakani Kasumulu Wilaya ya Kyela mkoani hapa wakitokea nchi jirani ya Malawi.

Mwisho.


No comments: