Monday, May 30, 2016

DAWASCO YAKANUSHA GARI YA DAWASCO KUJERUHI WATATU

Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO), imekanusha taarifa iliyoripotiwa na vyombo kadhaa vya habari juu ya gari linalodaiwa kuwa la DAWASCO lenye namba za usajili T 369 BUZ ambalo liliparamia kituo cha mabasi cha Mbuyuni kilichopo maeneo ya Namanga Oysterbay na kujeruhi watu watatu.
Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Meneja uhusiano wa Dawasco, Bi. Everlasting Lyaro amesema kuwa gari hilo sio mali ya Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es salaam, bali ni moja ya gari linalomilikiwa na watu binafsi   ambao wanasaidiana na Dawasco katika kusambaza huduma ya maji maeneo ambayo huduma hiyo bado haijafika kwa kutumia magari makubwa ya kusambaza Maji (maboza) ambayo yamesajiliwa na kuwekwa nembo ya Dawasco.
“Gari hili sio mali ya Dawasco, bali limesajiliwa na Dawasco na kuwekewa viambatanisho vyote muhimu  ili kusambaza huduma ya Maji maeneo ambayo mtandao wa Maji haujafika haujafika” alisema Lyaro.
Ikumbukwe kuwa mnamo mwezi Oktoba mwaka jana, Dawasco ilianza zoezi maalum la kusajili visima pamoja na magari yote makubwa ya kusambaza huduma ya Maji jijini Dar es salaam, ambapo tayari magari makubwa takribani 256 ya kusambaza huduma ya Maji jijini Dar es Salaam yamekwisha sajiliwa.
Dawasco inapenda kuvikumbusha vyombo vya habari kuzingatia taratibu za kazi kwa  kuandika taarifa zenye uhakika na ukweli ili kuepuka upotoshaji wa habari kwa wananchi.
Everlasting Lyaro
Kaimu Meneja uhusiano- Dawasco
022-2194800 au 08001164
Dawasco Makao Makuu
30/05/2016

No comments: