Sunday, August 20, 2017

UVCCM MKOANI SINGIDA WAMPONGEZA DC IKUNGI

BMG Habari, Pamoja Daima!
Umoja wa Chama cha Mapinduzi UVCCM mkoani Singida umempongeza Mkuu wa Wilaya ya Ikungi mkoani humo Mhe.Miraji Mtaturu kwa kuanzisha michuano ya Ikungi Elimu Cup 2017 ili kuhamasisha wananchi na wadau
mbalimbali kuchangia utatuzi wa changamoto za elimu kupitia Mfuko wa Elimu Ikungi.

Mwenyekiti wa UVCCM mkoani Singida, Jimson Mhagama (pichani) alitoa pongezi hizo jana Agosti 19,2017 kwenye uzinduzi wa michuano hiyo uliofanyika kwenye uwanja wa shule ya sekondari Ikungi mkoani Singida ambapo mgeni rasmi alikuwa Katibu Tawala mkoani Singida, Dkt.Angeline Lutambi aliyemwakilisha Mkuu wa mkoa huo Dkt.Rehema Nchimbi.

Uzinduzi wa michuano hiyo, ulikwenda sambamba na uzinduzi wa zoezi la ufyatuaji wa matofali kwa ajili ya ujenzi wa maabara uliokwama tangu mwaka 2009 katika shule ya sekondari Ikungi hii ikiwa ni uzinduzi rasmi wa zoezi kama hilo kwenye kata zote wilayani Ikungi ambapo kila Kata imepewa jukumu la kufyatua matofali elfu kumi kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na nyumba za waalimu.

Katika zoezi hilo, walijitokeza wadau pamoja na viongozi mbalimbali wakiwemo madiwani, wenyeviti wa halmashauri, jeshi la polisi, Tanesco na wanachi ambao walimuunga mkono Mkuu wa wilaya ya Ikungi, Mhe.Mtaturu aliyekabidhi mifuko 100 ya simenti na wao wakachangia fedha taslimu zaidi ya shilingi 800,000 na ahadi zaidi ya shilingi 1,900,000, ahadi za simenti mifuko 194 na mchanga wa moramu malori matano kutoka kwa mdau wa maendeleo wilayani Ikungi Hussein Sungita.

No comments: