Tuesday, September 28, 2010

JIKINGE AU JITIBU ‘PRESHA YA KUSHUKA ’ KWA CHAKULA

Wiki mbili zilizopita tuliwaletea mfufululizo wa makala mbili kuhusu ugonjwa wa presha ya kupanda (High Blood Pressure) ambapo tuliona namna gani watu tunatembea nao ugonjwa huo bila kujijua, licha ya ukweli kwamba unachukua uhai wetu kila siku. Halikadhalika tuliona aina mbalimbali za vyakula vinavyotoa ahueni ama kinga ya ugonjwa huo. Leo tunaangalia ugonjwa wa presha ya kushuka (Low Blood Pressure) ambao nao ni hatari kama ule wa presha ya kupanda, ukitofautiana kidogo namna unavyomsumbua mtu.

DALILI ZA MTU MWENYE PRESHA YA KUSHUKA
Mtu mwenye ugonjwa wa presha ya kushuka mara kwa mara husumbuliwa na uchovu, mwili kukosa nguvu, kuwa mnyonge na kusikia kizunguzungu. Hali hii hutokea baada ya mzunguruko wa damu kwenye mishipa kuwa mdogo kutokana na kupungua kwa msukumo wa damu hivyo viungo kama moyo, ubongo na viungo vingine kupungukiwa au kukosa damu kabisa.

SABABU ZA PRESHA YA KUSHUKA
Kwa mujibu wa wataalamu wetu wa masuala ya lishe, sababu kubwa inayochangia ugonjwa huu ni ukosefu wa virutubisho mwilini kunakosababishwa na ulaji usio sahaihi. Mtu anapokuwa na upungufu wa protini, vitamin C au moja kati ya Vitamin B hupatwa na tatizo hili. Aidha, ugonjwa wa presha ya kushuka, wakati mwingine husababishwa na kuvuja taratibu kwa damu mwilini kupitia kwenye utumbo, figo au kibofu. Mbali na matatizo hayo, pia hasira, kupatwa na msongo wa maisha na mawazo mengi, kunaweza kusababisha presha ya kushuka pia.

VYAKULA VINAVYOSAIDIA PRESHA YA KUSHUKA
Kwa mujibu wa watatifi wa vyakula, wamegundua kuwa juisi ya Bitiruti (beetroot) ina saidia sana mgonjwa anayesumbuliwa na ugonjwa huu. Bitiruti ni aina fulani ya viazi pori ambavyo vinabapatikana kwenye masoko mbalimbali nchini. Mgonjwa anashauriwa kutengeneza na kunywa kikombe kimoja cha juisi hiyo kutwa mara mbilli na anaweza kuona mabadiliko ndani ya wiki moja tu.

KUOGA MAJI YA CHUMVI
Dawa nyingine inayoweza kutoa nafuu na ya haraka kwa mgonjwa wa presha ya kushuka ni kuoga kwa kujiloweka kwenye maji ya chumvi maalum. Chukua kilo moja na nusu ya chumvi, kisha weka kwenye beseni kubwa la maji ya uvuguvugu, koroga kisha ingia ndani ya beseni hilo na ukae kwa dakika 10 hadi 20. Fanya hivyo muda mfupi kabla ya kwenda kulala na usipatwe na baridi.

VIRUTUBISHO KAMA TIBA
Protini, Vitamin C na Vitamin zote za kundi B, vimeonekana kuwa na uwezo mkubwa wa kutoa kinga au ahueni kwa wagonjwa wa presha ya kushuka. Mlo kamili wowote ulioshehemi vitamini B na virutubisho vingine, ni muhimu kuliwa na mgonjwa wa presha ya kushuka mara kwa mara.

Matumizi ya chumvi nyingi kwa mgonjwa wa presha ya kushuka nayo ni muhimu. Mgonjwa anashauriwa kula vyakula vyenye chumvi nyingi. Aidha, anaweza kunywa maji yaliyochanganywa nusu kijiko cha chumvi kila siku, hadi hapo kiwango cha presha yake kitakaporejea katika hali ya kawaida.

Ili kuliondoa tatizo la presha ya kushuka moja moja, mgonjwa wa presha ya kushuka anatakiwa kuzingatia ulaji wa matunda kwa kiasi kikubwa. Kwa kuanzia, anatakiwa kula mlo wa matunda-matunda tu kwa muda wa siku tano mfululizo, huku akila mlo huo mara tatu kwa siku ukipishana kwa umbali wa masaa matano.

Baada ya hapo, mgonjwa huyo anaweza kubadilisha mlo na ukawa wa matunda na maziwa kwa muda wa wiki mbili hadi tatu. Na baada ya hapo, anatakiwa kuzingatia ulaji wa vyakula asilia vyenye virutubisho vya kutosha ili kuimarisha mfumo wa damu mwilini. Na hii ndiyo iwe staili yake ya maisha kila siku, bila kusahahu mazoezi mepesi mepesi, yakiwemo yale ya kuvuta pumzi na kushusha.

No comments: