Saturday, February 18, 2012

Dr. JK aongoza matembezi ya kampeni ya "Moyo Challenge" Vodacom na CCBRT Jijini Dar es Salaam

 Rais wa Bodi ya Wakurugenzi wa Hospitali ya CCBRT Dk Wilbroad Slaa akisisitiza jambo kwa Ofisa Mkuu wa Masoko na Mahusiano wa Vodacom Tanzania Mwamvita Makamba kushoto na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Hospitali ya CCBRT Erwin Telemans katikati,wakati wa kampeni ya kutembea ya Moyo Challenge inahamasisha kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya CCBR kwa ajili ya kinamama wenye matatizo ya fistula waweze kupata huduma bure hapa nchini,Kampeni hiyo ilizinduliwa na Mh.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete leo jijini Dare s Salaam,Kwa kuchangia kwa njia ya M-PESA tafadhali tuma kwenda namba 200500,na kwa njia ya SMS tuma ujumbe mfupi usemao MOYO kwenda namba 15599.
 Rais wa Bodi ya Wakurugenzi wa Hospitali ya CCBRT Dk Wilbroad Slaa,akisalimiana na Kamanda wa kanda maalumu ya Dare s Salaam Suleiman Kova
 Mh.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Kikwete akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa kampeni ya kutembea ya Moyo Challenge
 Mh.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Kikwete akiongoza matembezi hayo
 Mh.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Kikwete akisikiliza jambo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania Rene Meza,kuhusiana na kampeni
Rais wa Bodi ya Wakurugenzi wa Hospitali ya CCBRT Dk Wilbroad Slaa amempongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kueleza kuwa katika masuala yanayohusu afya na uhai wa Mtanzania daima ameweka itikadi pembeni.

Dk Slaa ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema Rais Kikwete amepanda juu ya siasa katika masuala ya afya hata kama yanauhusiano na mtu wa upinzani katika siasa kwa kutambua kuwa wanaonufaika ni Watanzania na si chama fulani.

Kauli hiyo ya Dk Slaa aliitoa jana katika Hospitali ya CCBRT, Dar es Salaam kwenye kilele cha matembezi ya hisani kuchangia Sh bilioni Moja za ujenzi wa hospitali na tiba ya uzazi alipokuwa akitoa neno la shukrani kwa Rais Kikwete aliyekuwa mgeni rasmi.

Matembezi hayo ya hisani yalioandaliwa na kampuni ya simu ya Vodacom na CCBRT, yalianzia hoteli ya Golden Tulip saa moja asubuhi, umbali wa kilometa mbili na nusu hadi hospitalini hapo ikiwa ni sehemu ya Kampeni ya Moyo. Tangu kuzinduliwa kwa kampeni hiyo nchini wiki mbili zilizopita hadi jana zaidi ya Sh milioni 200 zimechangwa.

“Kabla hatujaanza matembezi, mwandishi alinifuata akaniuliza, Rais anakuja kwenye shughuli inayoongozwa na mtu wa upinzani? Unajua waandishi ni wachokozi, sikumjibu. Nimesema hili kuonesha kuwa hukujali nani ni nani, Rais umeonesha njia, umepanda juu ya siasa kwani fistula haina itikadi,” alisema Dk Slaa.

Akimmiminia sifa zaidi Rais na Serikali yake, Dk Slaa alisema Rais Kikwete ndiye aliyeongoza mchakato wa kufanikisha ujenzi huo mwaka mmoja na nusu uliopita, zikapatikana Sh milioni 500 wakati huo. Serikali yake ilitoa bure eneo la ujenzi pamoja na kuwepo tafrani za hapa na pale na pia kama haitoshi mara kadhaa amewatembelea kujua maendeleo yao.

“Hakuna kampeni kubwa unayoweza kufanya Mheshimiwa Rais kama hii, Serikali imekuwa ikilipa mishahara ya sehemu ya wafanyakazi wetu na kila mara ukija kututembelea kunapata ardhi, pengine na leo tutapata (kicheko),” alisema na kuongeza:

“Hizi zote ni juhudi za Serikali yao Mheshimiwa Rais, hakika inashirikiana nasi, kama hayo yote hayatoshi, umeamka asubuhi kutuongoza katika matembezi haya, tunaomba tuendelee hivi kuhakikisha ugonjwa huu unakwisha,” alisema Dk Slaa.

Awali katika hotuba yake, Rais Kikwete alisema kama alivyofanya kwa mapambano dhidi ya Ukimwi, anahamishia nguvu hiyo hiyo kwa fistula kwa kuandaa kampeni kubwa ngazi ya Taifa mpaka wilaya ili akinamama wenye fistula watibiwe na kurejesha utu wao kama wengine.

Alitoa onyo kwa wanaume wanaowapa talaka wake zao baada ya kuugua fistula kwamba kufanya hivyo ni kosa la jinai la kiutu, kwa kuwa ugonjwa huo ni matokeo ya mimba ambayo hakuipata peke yake bali yalichangiwa na mwanamume pia.

“Mimba ni matokeo ya tendo la furaha baina ya mume na mke, sasa mwenzako anapata fistula unampa talaka, kwani mimba aliipata peke yake (kicheko), hilo ni jambo la ovyo sana, wewe ndio ulihusika halafu unajidai kutoa talaka, ajabu sana hii,” alisema Kiwkete.

Akifafanua hilo, aliishuru CCBRT na Vodacom kwa kampeni hiyo na kuahidi kuwa serikali itaendelea kutoa elimu kwa jamii, wanaume na wanawake kutambua kuwa hakuna ushirikina katika fistula bali ni ugonjwa kama mwingine ili wajitokeze kupata tiba.

“Ninaiagiza wizara itengeneze kampeni hii ya Moyo kwa kushirikiana nanyi, tufanye nchi nzima, nimepiga kelele sana katika Ukimwi kwa gia ile ile sasa nahamia kwenye fistula, tuandae timu ya madaktari kama ni siku au wiki, tuende mpaka vijijini wanawake waweze kuhudumiwa,” alisema Kikwete na kushangiliwa.

Aliiomba Vodacom na CCBRT kuandaa tena matembezi kama hayo baada ya miezi sita ikiwa kiwango cha fedha hakitafikiwa huku akiahidi kuwa serikali itaendeela kutoa mchango wa fedha kuwezesha hospitali hiyo iliyotengwa maalum kwa huduma, iweze kuendelea kutoa huduma.

“CCBRT ni moja ya hospitali ambayo Serikali ni mbia nayo, tutaendelea kuwekeza ili kuiongezea nguvu, sasa moyo wangu baridiii, kwamba hospitali hii itajengwa, sit u itatibu fistula, lakini nimeambiwa magonjwa yaliyoshindikana ya uzazi yatatibiwa hapa,” alisema Rais Kikwete.

Kwa mujibu wa Vodacom na CCBRT, zaidi ya Sh bilioni 18 zinahitajika kuwezesha ujenzi huo utakaofanywa kwa miaka miwili, vifaa vya tiba na huduma ya bila malipo ya uzazi na fistula. Watu 14,000 watatibiwa kwa mwaka.

Hivi sasa wanawake 3,000 kila mwaka wanapata fistula na ni 1000 pekee wanapata tiba. Takwimu pia zinaonesha kuwa wanawake zaidi ya 24,000 wanaugua fistula nchini na lengo ni kuitokomeza ifikapo 2016.

Pamoja na kuishukuru Vodacom, CCBRT na makampuni ya Fodafone duniani kwa michango yao, Rais pia aliishukuru Jumuiya ya Ulaya (EU) na balozi mbalimbali kwa msaada wao katika afya hasa ya uzazi na kuwataka waendelee.

“Kwetu nchi za Afrika mwanamke akipata mimba tunaanza kuingiwa na hofu, tena ya kifo maana inageuka hatari kwa usalama wake na mtoto lakini kwa nchi zetu hili mmelifuta, pia masuala ya imani za kishirikina yanatusumbua, kitu kidogo ramli, hapa elimu zaidi tutaendelea nayo na wenzetu muendelee kusutusaidia,” alisema Rais Kikwete.

Aliwaomba Watanzania kujitokeza kuchangia kuanzia Sh 500 kwa njia ya simu za mikononi kwenda namba 15599 na ya M-Pesa namba 200500 ili kuwezesha hospitali hiyo kujengwa na tiba ya bila malipo kwa akina mama wenye fistula nchioni.

Kwa upande wake, akimkaribisha Rais kuhutubia hadhara hiyo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Haji Mponda alisema Serikali kupitia sera yake ya afya imeendelea kuboresha huduma kwa jamii hasa watoto na wajawazito na kuhusu fistula hospitali 25 za mikoa na 18 za mashirika ya dini zinatoa tiba hiyo nchini.

Mkurugenzi wa Makampuni ya Vodafone, Andrew Dunnet akizungumza katika hafla hiyo alisema nchi 25 duniani kupitia kampeni hiyo ya Moyo zinaendelea kuchangisha fedha za tayari zaidi ya Sh bilioni 10 zimechangwa.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Erwin Telemans, aliishukuru Serikali na Vodacom kwa mchango wao katika afya hasa kufanikisha matembezi hayo ya hisani. Alisema Vodacom imekuwa mstari wa mbele kupitia huduma ya M-Pesa hivyo ni wazi mwaka 2016, fistula itakuwa historia nchini.

Katika hafla hiyo, Rais alitoa vyeti kwa makampuni kadhaa yaliochangia kati ya Sh milioni tano hadi 10 katika kampeni hiyo jana. Rais mwenyewe alichangia Sh milioni tano na pia alitembelea eneo la ujenzi katika hatua ya msingi. Pia kabla alitembeela wodi ikiwemo ya wagonjwa wa fistula.

No comments: