Thursday, July 26, 2007

O-TEN AIBUKA TENA



Kutoka mkoani Morogoro, ShowBiz ilifanikiwa kupiga stori na msanii Philipo Nyandidi O-Ten ambaye hivi sasa amerudi upya katika game, aliyetamka kwamba hawezi kuizungumzia ishu ya kujitoa katika familia ya East Coast Team kama walivyofanya baadhi ya wasanii wenzie kwa sababu hakuwa na mkataba wowote katika umoja huo.

Msanii huyo alisema kwamba yeye alikuwa ndani ya umoja huo kiushikaji tu, wala hakuna mkataba wowote aliosaini ambao ungemzuia kuondoka au kuendelea kuwepo katika familia hiyo, kitu ambacho anapenda watu wakielewe, hasa wale waliokuwa wanasubiri kauli yake kuhusu kujitoa kama walivyofanya A.Y, Mwana FA na Buff G.

“Nisingependa kusema nimeondoka ECT kwa kuwa nilikuwa pale kwa kampani tu, bado naendelea kufanya kazi zangu kama mimi, pia natoa nafasi kwa mtu yeyote atakayependa kufanya mikataba na mimi ambayo itakuwa na faida katika maisha yangu” alisema Nyandidi.

Akiuzungumzia ujio wake mpya O-Ten alisema kwamba alichokifanya katika wimbo huo wenye jina la ‘Uko Wapi’ ni mabadiliko ambayo yatawashangaza watu wengi. “Mashabiki wanaweza wasiamini kama ni O-Ten yule yule waliyemzoea au mwingine, kwa sababu nimefanya mapinduzi makubwa katika sanaa!”

Kazi hiyo mpya ya O-Ten ambayo inamrudisha kwenye game imewashirikisha wasanii Nonini wa Kenya na A.Y. kutoka Bongo. Zoezi la kukamilisha kazi wimbo limefanyika nchini Kenya kupitia studio za Ogopa Dj.

No comments: