Monday, September 27, 2010

WIKIENDA SHOWBIZ!

P. Funk: Bongo Records ni ofisi, si uwanja wa ngumi
Ukiwa pande za Nanjilikitili halafu unasikia sifa za Bongo Records unaweza kudhani ni studio iliyopo kwenye eneo kubwa kama Kariakoo nzima.

Anayepunguza, basi ataamini ni go-down kubwa halafu ndani yake kuna mitambo ya nguvu, Mkurugenzi Mtendaji wake, Paul Matthysse ‘P. Funk’ analindwa na wapambe 50, ukithubutu kumsogelea umeumia.

Bongo Records ina jina kubwa. Ambao hawajawahi kuiona halafu wanaifikiria kwa ukubwa wa kupitiliza wana sababu ya kuifikiria kwa ukubwa huo.

Imewatoa wakongwe wengi tu, Juma Kassim Kiroboto ‘Nature’, Juma Mchopanga ‘Jay Moe’, Albert Mangwea ‘Ngwair’ na Jaffari Mshamu ‘Jaffarai’ na wengine wengi.

Mafanikio ya Joseph Haule ‘Prof. Jay’, Haroun Kahena ‘Inspector’ na Gangwe Mob, Wanaume Family na Halisi na utitiri wa wasanii wengi, kwa namna moja au nyingine, Bongo Records na mkono wa P. Funk ‘Kinywele Kimoja’ vimefanya waking’ara.

Tukumbuke kuwa kipindi kirefu Bongo Records ilibaki kuwa mtawala wa soko la Bongo Flava, ingawa kwa nyakati tofauti kulikuwa na ushindani na MJ Production ya Joachim Kimaryo ‘Master J’ na FM Studio wakati huo Mika Mwamba anasababisha.

Hata hivyo, kinachoonekana hapa ni kuwa P. Funk anashindwa kuiheshimu studio yake wala hajali ukubwa wa jina lake na ndiyo maana anakuwa na migogoro ya hapa pale na wasanii ambao wanakwenda kurekodi.

Ukiachana na vilio vya wasanii chipukizi, hata wakongwe nao imeonekana kasi yao ya kwenda studio hiyo imepungua. Kuna tatizo! Ipo sifa inayoenea mtaani kwamba P. Funk ni master wa kusimamia vipaji, kwamba wale ambao hawawezi huwa haoni mbaya kuwatoa nishai. Hataki tu kuchukua pesa ya mtu, anaangalia kwanza kazi anayotengeneza. Anahitaji pongezi!

Hilo sawa lakini migogoro na wasanii wake ya nini? Mastaa wengi wanamuogopa kwa sababu dakika mbili mbele anaweza kubadilika na kufanya kitu cha kushangaza.

Ijumaa iliyopita, Mfalme wa Rhymes, Suleiman Msindi ‘Afande Sele’, alipita ofisini kwetu akiwa na furaha. Alikuja kutusabahi na baada ya hapo alitupa taarifa kwamba anakwenda Bongo Records kuchukua kazi yake kwa Majani.

Kwamba walikubaliana aende siku hiyo kazi yake ambayo Afande alirekodi na staa wa Ninao Ninao, Ferouz Mrisho Rehani. Dakika 10 nyingi, Afande akawa anazungumzia Kituo cha Polisi kwamba amekwenda kumfungulia mashtaka P. Funk kuwa alimtukana, akampiga kofi na kumtishia bastola.

Hilo ni moja la Afande na hatuwezi kuingia ndani zaidi ya kesi hiyo kwa sababu kada za sheria zinazohusika zitafanya uamuzi lakini hapa tunatoa ushauri kiduchu kwa P. Funk.

Aheshimu studio yake kama kweli muziki ni kazi yake. Migogoro na wasanii hatakiwi kuipa nafasi, zaidi studio iwe sehemu ya heshima (ofisi), siyo eneo ambalo wakati wowote linaweza kugeuzwa ringi ya ngumi.
********************
Blu: Aufuata mfupa uliomshinda Ray C
Bongo Flava legend, Hery Samir ‘Blu’ yupo njia moja kutua nchini Kenya ambako atagonga shoo ya pamoja na staa wa Kidato Kimoja, Juma Issa ‘JI’.


Blu, amepewa dili na promota maarufu Kenya, Sadat Muhindi ambaye hivi karibuni alizinguana na diva wa Bongo Flava, Rehema Chalamila ‘Ray C’.

Kwa mujibu wa Sadat kama alivyozungumza na kona hii wiki iliyopita, Blu atapiga shoo na JI katika shoo maalum ya kulipiga promo Kundi la Maliza Umaskini.
Alisema, Oktoba 8, 2010 Blu na JI watasimama jukwaa moja mjini Embu ambao upo kilomita 120 (maili 75) kutoka Mji Mkuu wa Kenya, Nairobi.

Sadat alisema, baada ya shoo hiyo, siku inayofuata (Septemba 9), Blu atadondoka Nakuru na katika shoo zote hizo, Maliza Umaskini Family (MUF) watapanda jukwaani na kufanya onesho moja.

Maliza Umaskini ni mradi wa kupambana na makali ya maisha ambao umeanzishwa na Sadat nchini humo na katika kuupiga promo, promota huyo aliingia makubaliano na Ray C lakini walitofautiana na kuvunja mkataba.
***************************************************************

-Ipo siku Nick Minaj atatoana roho na Lil Kim, Foxy Brown
-Mambo yanazidi kukolea, upande mwingine Lil Kim naye ni chuki dhidi ya P Diddy na mkwewe, mama Notorious BIG
Nick Minaj
Nick Minaj
Rapa wa kike anayefanya vizuri zaidi dunini, Onika Tanya Minaj a.k.a Nicki Minaj yupo kwenye bifu la kutisha na mkongwe, Kimberly Denise Jones ‘Lil Kim’.


Bifu la Nicki na Kim limezidi kukolea siku baada ya siku, huku upande mmoja ukionekana kurusha makombora zaidi. Ikionekana Kim anasaka shari, kabla hajamalizana na Nicki, amewarudi Sean Combs ‘P Diddy’ na mkwewe, mama wa legend wa Hip Hop duniani, Christopher Wallace ‘Notorious BIG’, Voletta Wallace.

CHANZO BIFU LA NICK, KIM
Wigi ni alama ambayo imekuwa ikimtambulisha Kim tangu alipoanza kuuza jina lake kwenye muziki wa Hip Hop miaka ya 1995/1996.


Wakati huo, akitambulika kama first lady wa Kundi la Junior M.A.F.I.A pia malkia wa lebo ya Bad Boy Entertainment, Kim alitaka ajulikane kwa mikato yake mbalimbali lakini mwisho wa yote kichwani alimaliza kwa wigi.

Kuonesha kwamba wigi ni nembo ya Kim, katika video ya Hit em Up, Mfalme wa Hip Hop duniani, Tupac Shakur ‘Makaveli the Don’ anaonekana akimvua wigi mrembo aliyemchezesha mfano wa first lady huyo wa Junior M.A.F.I.A.

Nicki alipoanza kutoka, moja kwa moja naye akavamia staili ya kuupara wigi kichwani, Kim akaona hee: “Dogo anaingia kwenye anga zangu!”

Vurugu zikawa zinazagaa kitaani, chini kwa chini ikaelezwa kwamba Nicki aliamua kutoka na wigi kwa sababu ujio wake una maana moja kubwa muhimu, kumfunika moja kwa moja Lil Kim.

Kwa upande mwingine, Lil Kim yeye akawa anafyatua madongo ya wazi kuwa Nicki ni mdogo na hajiwezi, kwahiyo ni aibu kutaka kujifananisha naye.

KIM ALIVYOMCHANA NICKI BUFFALO
Katika shoo yake kwenye Ukumbi wa Buffalo, New York, Marekani Kim alitangaza kuwa anakwenda levo nyingine kwa sababu kuna kidudu mtu anamfuatafuata.


Kim alivua wigi na kuwatupia mashabiki kisha akadai kwamba analipenda lakini ni lazima aende matawi mengine kwa sababu hawezi kufanana na mtu ambaye inaaminika ni Nicki.

“Naenda levo nyingine,” Kim aliwaambia mashabiki wake. “Napenda wigi na kila kitu lakini mimi nipo juu sana ya hili. Nipo juu sana ya hili… nitarudi tena!”

RAY J, KIM WAMSHAMBULIA NICK
Akionesha kwamba hataki kimwana wake achokozwe, Willam Raymond Norwood ‘Ray J’ alipiga dongo kwa Nick wazi wazi kuwa hawezi kuwa sawa na Lil Kim.


Ilikwishawekwa wazi kwamba Ray J ambaye ni kaka mdogo wa staa wa R&B, Brandy Norwood ni mpenzi wa Kim, hivyo kuingia kwake kwenye vita hiyo ni wazi yanakuja mengine.

NI TISHIO LA TUPAC, BIGGIE WA KIKE
Jinsi mgogoro wao unavyokua ndivyo hofu kwamba si ajabu tunapoelekea, Kim na Nicki watarudisha kumbukumbu ya Tupac na BIG ambao mwisho wao kila mmoja ulikuwa kifo cha risasi. Wanazidi kuufanya umma uamini kuwa Hip Hop ni muziki wa fujo kwa sababu bifu kila siku zinaibuka, ingawa wengine hutetea kwamba ni biashara lakini mbona wanauana?

KIM VS P DIDDY & MAMA BIG
Kim kwanza hakubaliani na uundwaji wa filamu ya Notorious ambayo inaelezea maisha ya BIG. Mwana Hip Hop huyo anadai kuwa yeye kama mmoja wa washirika wa matukio muhimu ya BIG katika maisha yake alipaswa kushirikishwa. Analaumu pia kwamba muigizaji, Naturi Naughton ambaye amecheza kama yeye katika filamu hiyo, amemdhalilisha kwahiyo filamu nzima imemchafua.

Katika moja ya intavyuu zake, Kim analaumu kuwa filamu hiyo ni mchezo wa P Diddy na mama yake BIG, kutaka kujipatia fedha. Analaumu kuwa wameamua kwa makusudi kuchafua image yake ili kujipatia fedha.

Hata hivyo, Kim anasifia idea ya filamu hiyo na kuongezea kuwa endapo angeshirikishwa kama ambavyo uhalisia wake umetumika, angeweza kuboresha kwa namna nyingi.

Moja kati ya matukio ambayo yamemuudhi Kim ni pale ambapo mtu aliyeigiza kama yeye (Naturi) anaonekana studio akiwa anaingiza sauti, halafu prodyuza, Jamal Woolard aliyehusika kama BIG, anamkumbatia kwa furaha na kumbusu mkewe, Antonique Smith (kama Faith Evans).

Kwa uhalisia, BIG alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Kim lakini baadaye alifunga ndoa na Faith moja ya vitu ambavyo viliibua mtifuano mkubwa miaka hiyo.

Kim anaamini tukio hilo kwamba yeye yupo studio anaingiza vocal halafu BIG anamkubatia na kumbusu Faith, halafu yeye anasita lakini baadaye BIG anamkaripia kwa kumwambia aendelee, limemdhalilisha.

NICKI VS FOXY BROWN
Hayupo kimya na anadisi kwa sana tu! Nicki anawaponda wakongwe wa kike ambao mwisho wa siku inatafsiriwa kuwa madongo ni wazi kwa Lil Kim na Inga D. Marchand ‘Foxy Brown’.


Nicki anarap: “Makahaba wa zamani wanabadili meno yao ya bandia, nilipoingia kwenye game wote wakachezea benchi, na huo urafiki wenu mbuzi naona mnanifuatilia.”

Mistari ya Foxy Brown: “Nawaua hao, nawaua hao, naupoteza upinzani wa kibwege nawaua.” Nicki ameijibu: “Unawaua, unawaua, wewe kahaba mbona mimi nimeshawaua?”

NICKI ALIPOTOKA
Alianza kusugua kwenye mixtapes lakini akapata ngekewa ya kuuza sura kwenye jarida la XXL. Mwaka 2008 alishinda tuzo ya Mwanamuziki Bora wa Kike chipukizi ambazo zilitolewa na Undeground Music Awards.


Nicki pia alitoa Bean Me na Up Scotty kwenye mixtape nyingine na April 2009 zilipokelewa vizuri BET na MTV. Mwaka huu, alitoka na albamu yake ya kwanza Pink Friday na wimbo Your Love ndiyo uliomtambulisha vema kwa kupata airplay ya kutosha na kufika namba 14 katika Chati za Billboard Hot 200.

Alishirikiana na wana wa lebo yake ya Young Money kutoa albamu ya ushirika ambayo inaitwa We Are Young Money mwaka 2009. TUZO BET 2010 alibeba nne ambazo ni Mwanahip Hop Bora wa Kike, Msanii Bora Mpya, Kundi Bora (Young Money) Kundi Bora Jipya (Young Money), pia alipendekezwa kipengele cha Chaguo la Watazamaji akashindwa. MTV alipendekezwa kwenye kipengele cha Chaguo la Watazamaji, alipendekezwa pia Teen Choice Awarrds na Mombo Awards.

HUYU NDIYE MPENZI WAKE
Anahusishwa kutoka kimapenzi na mkali wa Hip Hop, Dwayne Michael Carter ‘Lil Wayne’ lakini uhusiano ambao unatambulika ni ule kati yake na mwanamuziki wa lebo za Young Money na Cash Money, Aubrey Graham ‘Drake’.

compiled by Mc Geroge/Ijumaa Wikienda

No comments: