Monday, July 16, 2007

TUNAOMBA KUWASILISHA HOJA: UKIMWI SIYO UGONJWA BALI NI HALI!


Pichani ni mwanaharakati maarufu wa masuala ya Ukimwi nchini Tanzania, Bw. Joseph Katto. Hakika anapaswa kuwa mfano wa kuigwa na mtoa matumaini kwa waathirika wengine wa Ukimwi nchini Tanzania na dunia nzima kwa ujumla, anaishi na virusi vya HIV kwa mika 20 sasa!

Mwishoni mwa wiki iliyopita,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Jakaya Mrisho Kikwete alizindua kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha Watanzania kupima afya zao, ili kujua kama wana virusi vya HIV ama la. Katika hili hatuna budi kumpongeza sana kiongozi wetu na kumuunga mkono kwa sisi wadau kuendelea kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi juu ya dhana hii ya ukimwi.
Kwa maombi mengi ya wasomaji wetu, leo tunarudia mjadala huu kama tulivyokwisha andika miezi kadhaa iliyopita katika gazeti la UWAZI kuwa ukimwi siyo ugonjwa, kama ambavyo watu wengi wanavyoelewa, bali ni hali ambayo mtu huipata kabla ya kuanza kuugua ugonjwa fulani, baada ya kinga yake ya mwili kushuka. Na je, kuna uhusiano gani kati ya ukimwi na lishe bora?

Kabla hatujaendelea, kwanza tujiulize ukimwi ni nini? Watu wengine wanaposema fulani ana ukimwi wana maanisha nini, na sisi tunaposema ukimwi si ugonjwa bali ni hali, tunamanisha nini?
UKIMWI ni kifupi cha maneno ya Upungufu wa Kinga Mwilini, hiyo ndiyo tafsiri rasmi tunayoambiwa na wataalamu wetu wa masuala ya ukimwi nchini, ambayo imetafsiriwa kutoka katika maneno ya kiingereza ya AIDS (Acquired Immune Deficiency Syndrome).Kwa mtizamo wetu, tafsiri yetu ya kiswahili haikujitosheleza sawaswa kama ile ya kiingereza, kwani limekosekana neno muhimu sana , ‘dalili za ugonjwa’ (Syndrome), ambalo lingetoa tafsiri halisi ya neno AIDS. Lakini pengine wataalamu wetu waliamua kuliacha neno hilo kwa sababu maalum, pengine lisingeweza kutamkika kirahisi.Hivyo tafsiri sahihi ya AIDS ilipaswa kuwa Dalili za Upungufu wa Kinga Mwilini (DAUKIMWI). Hivyo tunaposema fulani ana ukimwi, tuna maana ameanza kuonesha dalili kuwa ana upungufu wa kinga mwilini mwake kwa kuanza kuugua ugonjwa mmoja au zaidi.

Sasa mtu anaupataje ukimwi? Mtu anaweza kuipata hali hiyo kwa kupitia njia mbili. Mosi kwa njia ya kuambukizwa virusi viitwavyo HIV ambavyo kazi yake ni kuharibu mfumo wa kinga ya mwili. Njia ya pili ni kukosa kula lishe bora. Hivyo basi siyo wote wenye ukimwi wana HIV, wapo wenye ukimwi lakini hawana HIV, na wapo wenye HIV lakini hawana ukimwi, soma hoja hii kwa makini!
Mwili wa binadamu unalindwa dhidi ya maradhi na kitu kinachoitwa ‘kinga ya mwili’ (Body Immunity) ambayo kila binadamu anayo, lakini inatofautiana kiwango kutokana na mtu anavyokula au anavyoishi. Ulaji wako ukiwa mbaya, kinga yako nayo itakuwa mbaya, ulaji wako ukiwa mzuri, kinga yako nayo itakuwa nzuri.Ukiwa na kinga nzuri ya mwili, huwezi kuugua mara kwa mara malaria, mafua ya muda mrefu, kukohoa kwa muda mrefu, kifua kikuu, mkanda wa jeshi, kutokwa na vipele mdomoni, n.k. Ukiwa na kinga dhaifu, magonjwa niliyoyataja hapo juu na mengine hatari, yatakupata mara kwa mara.

Kutokana na ukweli huo, inapotokea mtu ameenza kusumbuliwa na maradhi ya mara kwa mara, mara nyingi hushauriwa kwenda kupima kama ameambukizwa virusi vya HIV, baadhi hukutwa hawana na kubaki wakijiuliza kwa nini wanaumwa mara kwa mara?

Ukienda kupima na kisha ukaambiwa huna virusi vya HIV, lakini afya yako siyo nzuri, basi elewa wewe tayari una ukimwi (Sio HIV Positive) na tiba pekee ni kula vyakula sahihi vitakavyokurejeshea kinga yako ya mwili ya asili ambayo itapambana na hayo maradhi na kuyatokomeza kabisa, na wala siyo suala la kula dawa kutwa mara tatu!

Halikadhalkika, kuna wengine ambao husumbuliwa na maradhi ya mara kwa mara, na wanapokwenda kupima, hukutwa tayari wameambukizwa virusi vya HIV.
Mara nyingi ushauri wanaopewa watu wenye virusi, ni kula vyakula bora, kama vile matunda, mboga za majani, maharage, vyakula vitokanavyo na nafaka zisizokobolewa na vyakula vingine vingi vyenye virutubisho vya kutosha, ushauri ambao ndiyo muhimu zaidi kuliko hata kuanza kutumia vidonge (ARV’S).Lakini katika kundi la watu ambao tayari wameambukizwa virusi, usishangae ukawakuta ambao afya zao ni nzuri na wala hawaugui maradhi ya aina yoyote, kama vile tulivyomuona na kumsikia wiki iliyopita katika viwanja vya Mnazi Mmoja Dar es salaam Bw. Joseph Katto ambaye amekuwa akiishi na virusi vya HIV kwa miaka 20 sasa. Hawa ina maana kinga zao za mwili zi ngali imara kutokana na vyakula wanavyokula na sataili ya maisha wanayoishi.Bw. Katto ni mfano mzuri wa kuigwa kwa watu wote wanaojali afya zao, hasa wale ambao wamepewa majibu yanayoonesha tayari wameathirika. Bila shaka ukimuuliza Bw. Katto siri ya afya yake njema atakwambia iko kwenye lishe zaidi kuliko vidonge na kubadilisha staili ya maisha kwa kuishi kama vile ambavyo mwili unavyotaka, na siyo kama nafsi yako inavyotaka.

Hivyo basi kama utaweza kuimarisha kinga yako ya mwili kwa ulaji sahihi, virusi vina kazi ngumu sana ya kuishinda na kuiharibu kinga yako ya mwili ya asili. Kwani kinga yako ya mwili ikiwa imara, ina kuwa ni sawa na kuviweka virusi nje ya uzio wa nyaya zenye miba (barbed wire) ambako havitaweza kupita.

Kwa mujibu wa watafiti wa masuala ya ukimwi, hatari ya virusi vya HIV (Human Immunodefiency Virus) katika mwili wa binadamu ni uharibifu vinaoufanya katika seli za mfumo wa kinga ya mwili (Human Immune System), ambapo huharibu au kuzuia seli kufanyakazi zake ipasavyo. Lakini kwa kula lishe bora, virusi hivyo vinakuwa na kazi ngumu ya kupenya ngome ya ulinzi kuzifikia seli hizo.

Kwa mantiki hiyo, ukimwi siyo ugonjwa, bali ni hali inayompata mtu kutokana na kukosa vyakula vya kujenga kinga ya mwili. Unaofikia hatua ya kupungukiwa kinga ya mwili, yaani kuwa na ukimwi, ndipo ugonjwa hujitokeza. Ugonjwa huo unaweza kuwa wowote ambao ulikuwa ukikunyemelea kwa mura mrefu kutokana na staili ya maisha unayoishi.

Baada ya kuwa na ukimwi, wengine hushikwa na kifua kikuu, wengine hupatwa na kiharusi na kupooza mwili, wengine hushikwa na ugonjwa wa moyo na kufa ghafla, wengine hupatwa na majipu au vipele mwili mzima na wengine hupatwa na madonda koo yanayowafanya washindwe kula na hatimaye kufa.
Kwa mantiki hiyo, siyo sahihi kusema fulani amekufa kutokana na ugonjwa wa ukimwi. Lazima kunakuwa na ugonjwa ambao unajulikana lakini umeshindwa kutibika kutokana na mtu huyo kutokuwa na kinga yoyote ya mwilini. Hivyo mtu mwenye virusi vya HIV hupata ukimwi kwanza kisha baadae ndiyo huugua ugonjwa ambao hatimaye hukatisha maisha yake!

Natumaini hoja yangu imeeleweka, kama haijaeleweka au kuna nyongeza, nakaribisha mjadala.

No comments: