Wednesday, December 7, 2011

Pima-Maji Ya Mjengwablog: January Makamba Na 'Mo' Dewji Wanakwenda Vizuri

Ndugu zangu,
Siku ya pili ya kupiga kura kwenye Pima-Maji ya
mjengwablog.com inamalizika saa chache zijazo. Mwitikio wa wapiga kura ni mkubwa kuliko ilivyotarajiwa. Takribani watu mia sita wamepiga kura ndani ya saa 48.

Tafsiri ya kura zilizopigwa hadi sasa:


John Mnyika na Zitto Kabwe wana command kubwa ya wafuasi. Ninavyoandika sasa Zitto Kabwe anaongoza kwa kura nne tu dhidi ya John Mnyika. Na wote wawili wanatarajiwa kuweka rekodi ya kukusanya kura zaidi ya mia mbili kwa kila mmoja ndani ya saa 48.


Godbless Lema:


Mwanasiasa huyu kijana bado yuko kwenye nafasi ya tatu. Anakuja kwa kasi ingawa anaonekana kutokuwa na command kubwa kwa wapiga kura wa kada ya kati. Ndio, katika siku mbili hizi ' Mandela effect' haijamsaidia sana Lema kwenye kura hizi.


January Makamba na ' Mo' Dewji:


Wakati vijana wengine ndani ya CCM wakiwa wamefunikwa na vumbi la ' Mbio za Urais 2015' January na ' Mo' Dewji wanaonekana kwenda vizuri katika kura hizi za mtandaoni. Bila shaka wameweza kujipambanua, hivyo basi, kuonekana na hata kuheshimika na vijana walio upande wa upinzani na ndani ya chama chao. Vijana ambao, kwa wakati huu wanaonekana kukipa mgongo Chama Cha Mapinduzi.Kama CCM itawapeleka mbele January na ' Mo' Dewji, basi, yawezekana wakachangia kwenye kujenga kwa vijana, image chanya kwa chama chao .


Mr. Sugu?


Naam, Mr. Sugu ni Mr. Sugu, ni ' Street Fighter'. Ni maarufu kisiasa kwa sasa, ingawa, naye haonekani kuwa na command kwa watu wa kada ya kati. Hata hivyo, kura za Mr. Sugu zimeanza kupanda. Yawezekana habari za uwepo wa shughuli hii ya kupiga kura za mtandaoni zimeanza kuwafikia ' Wasela' wake ' In The Streets'.


Jokeli kwenye mchakato?


Kuna mbunge kijana anaitwa Livingstone Lusinde.


Kwenye mchezo wa karata kuna jokeli. Karata hii jokeli huwa haihesabiki lakini inaweza kuamua mchezo wa karata inapotupwa kwa wakati sahihi na mahali sahihi.


Mbunge Lusinde ndiye ambaye mpaka sasa hana kura hata moja. Ana sifuri. Kwamba hata yeye mwenyewe hajajipigia, au labda kajichimbia jimboni Mtera kusiko na kompyuta. Naam, kura ya Lusinde anaweza asijipigie mwenyewe akaja kumpigia Mnyika au Zitto na ikaamua mshindi!


Zimebaki siku tisa za kupiga kura. Nenda
http://mjengwablog.com ukampigie kura mbunge wako kijana unayeona yuko juu.

Maggid Mjengwa,


Mratibu.

http://mjengwa.blogspot.com

No comments: